SIMBA SC YAWANIA TAJI LA 40 LEO

Unknown | 8:04 AM | 0 comments


Na Mahmoud Zubeiry, Zanzibar
TIMU ya soka ya Simba SC, leo inawania taji la 40 tangu ianzishwe mwaka 1936, wakati itakapomenyana na KCC ya Uganda katika Fainali ya Kombe la Mapinduzi, Uwanja wa Amaan, Zanzibar.
Timu hiyo maarufu kama Wekundu wa Msimbazi, ilianzishwa mwaka 1936, enzi hizo ikijulikana kwa jina la Queens, yaani Watoto wa Malkia, kabla ya baadaye kubadilisha jina na kuwa Eagles, yaani ndege aina ya Tai, jina ambalo halikudumu sana nalo likatupwa na kuwa Sunderland, ambalo lilidumu hadi mwaka 1971 lilipobadilishwa na kuwa Simba SC hadi leo.
Kikosi kazi; Kikosi cha Simba SC katika Kombe la Mapinduzi  

MATAJI YA SIMBA SC

UBINGWA WA LIGI KUU:
1965, 1966, 1973, 1976, 1977, 1978, 1979, 1980, 1984, 1990, 1994, 1995, 2001, 2003, 2004 na  2007 (Ligi Ndogo), 2010 na 2012.
KOMBE LA NYERERE:
1984, 1995 na 2000 
KOMBE LA MUUNGANO:
1993, 1994, 1995, 2001, na 2002
KOMBE LA TUSKER:  
2001, 2002, 2003 na 2005 
KOMBE LA KAGAME:
1974, 1991, 1992, 1995, 1996 na 2002
KOMBE LA MAPINDUZI:
2008 na 2011
KOMBE LA MTANI JEMBE:
2013: 
Sababu ya kuachana na jina la Sunderland ni aliyekuwa Rais wa Kwanza wa Zanzibar, Abeid Amaan Karume (sasa marehemu), ambaye wakati anaweka jiwe la msingi kwa ajili ya ujenzi wa jengo la klabu hiyo, lililopo Mtaa wa Msimbazi, mwaka 1971, alikemea tabia ya kupenda kuiga mambo ya Waingereza, akiamini kufanya hivyo ni kuendelea kuutukuza ukoloni.
Rais Karume, aliwaambia Simba waachane na majina ya kizungu na watumie jina la asili ya Afrika na ndipo jina la Mnyama tishio zaidi porini, Mfalme wa Nyika, Simba, lilipowavutia hata ukawa mwanzo wa Simba SC tishio hii ya leo, inayomtesa mtani wake, Yanga SC.
Katika kipindi chote cha uhai wa klabu hiyo, imetwaa Kombe la ubingwa wa Ligi Kuu ya Bara mara 18, Kombe la Nyerere mara tatu, Muungano mara tano, Tusker mara nne, Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, maarufu kama Kombe la Kagame mara sita, Nani Mtani Jembe mara moja na Mapinduzi mara mbili, hayo yakiwa ni jumla ya mataji 39.
Leo Wekundu wa Msimbazi wanataka kuweka rekodi ya kutimiza mataji 40 Uwanja wa Amaan, mbele ya Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Shein, mchezo utakaoanza Saa 10:00 jioni.
Kikosi cha KCC ya Uganda kilichowavua ubingwa Azam FC

WANAOWANIA UFUNGAJI BORA KOMBE LA MAPINDUZI

Owen Kasuule URA  4
Amri Kiemba Simba SC 3
Feni Ali   URA  3
Rama Singano Simba SC 2
Tony Odur KCC  2
Brian Umony Azam FC 2
Jose Kimwaga Azam FC 2
M. Mngwali Chuoni 2
H. Waswa KCC 2
Mechi ya leo inazikutanisha kwa mara ya pili Simba SC na KCC, timu ya Mamlaka ya Jiji la Kampala, baada ya awali pia kukutana katika mchezo wa Kundi B na kutoka sare ya bila kufungana.
Kocha wa Simba SC, Zdravko Logarusic amesema kwamba amewaandaa vyema vijana wake kuelekea mchezo wa leo na watapigana kufa na kupona dhidi ya timu bora ya Uganda ili kupata matokeo mazuri leo.
“Itakuwa mechi ngumu sana, hii ni fainali. Wazi ni mechi tofauti sana na zile zilizotangulia, unacheza unaliona Kombe na unataka kulibeba, nimezungumza sana na vijana wangu, naamini hawataniangusha,”alisema Logarusic raia wa Croatia, ambaye mwezi uliopita aliipa Simba taji la kwanza, Mtani Jembe kwa kuwafunga watani, Yanga 3-1.
Kipa wa Simba SC, Ivon Philip Mapunda ‘Ivo’ amedaka mechi nne za mashindano haya bila kufungwa hata bao moja na bila shaka leo atataka kumaliza michuano bila kumbukumbu ya kuokota mpira nyavuni ili pia kujitengenezea mazingira ya kuwa kipa bora wa Kombe la Mapinduzi 2014.
Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba SC, Zacharia Hans Poppe akiwa ameinua taji la 39, baada ya kuifunga Yanga 3-1 Desemba 21 mwaka jana katika mechi ya Nani Mtani Jembe. Je, leo atainua taji la 40?  
Kiungo Amri Ramadhani Kiemba amefunga mabao matatu hadi sasa kwenye mashindano haya, anazidiwa bao moja tu na mchezaji anayeongoza, Owen Kasuule wa URA ya Uganda iliyotolewa na Simba SC katika Nusu Fainali.
Ramadhani Yahya Singano ‘Messi’ amecheza vizuri katika mechi zote nne alizopangwa na hadi sasa ni kati ya wachezaji wanaotazamiwa kutwaa tuzo ya mchezaji bora wa mashindano.
Wachezaji hawa watatu, Mapunda, Kiemba na Messi hakika leo wanatarajiwa kuwa chachu ya matokeo mazuri kwa Simba SC- mbele ya KCC yenye matumaini makubwa ya kuondoka na Kombe la Mapinduzi.  
Kampuni ya CXC Safaris & Tours ya Dar es Salaam, chini ya Mkurugenzi wake, Charles Hamkah inatarajiwa kutoa Sh. 300,000 kwa kila mmoja, mfungaji bora, mchezaji bora na kipa bora. 
Hii ni michuano ya nane ya Kombe la Mapinduzi inayokuja sambamba na sherehe za miaka 50 ya Mapinduzi ya Zanzibar tangu kung’olewa kwa utawala dhalimu wa kisultani visiwani hapa. 
Timu tano zimetwaa Kombe hilo tangu limeanzishwa mwaka 2007, Yanga SC ya Dar es Salaam ikikata utepe, ikifuatiwa na watani wao, Simba SC (2008), Miembeni ya hapa (2009), Mtibwa Sugar ya Morogoro (2010), Simba SC tena 2011 na Azam FC mara mbili mfululizo 2012 na 2013.
Mabingwa watetezi, Azam safari hii wamekwama kwenye Nusu Fainali baada ya kutolewa na KCC kwa kufungwa mabao 3-2, ikitoka nyuma kwa 2-0. 
Kocha Logarusic mbele wakati wanapokea Kombe la Nani Mtani Jembe Desemba 21
Katika mchezo wa leo, unaotarajiwa kuchezeshwa na refa mwenye beji ya FIFA, Ramadhani Ibada ‘Kibo’, vikosi vya timu zote vinatarajiwa kuwa; 
Simba SC; Ivo Mapunda, Haruna Shamte, Issa Rashid ‘Baba Ubaya’, Donald Mosoti ‘Beki Adui’, Joseph Owino, Jonas Mkude, Haroun Chanongo, Amri Kiemba, Amisi Tmbwe, Ramadhani Singano ‘Messi’ na Awadh Juma.
KCC; Omar Magoola, Saka Mpima, Habib Kavuma, Ibrahim Kiiza, Fahad Kawooya, Gadafi Kiwanuka, Herman Wasswa, Tom Masiko, Tony Odur, Stephen Bengo na William Wadri. 

Share story hii kupitia>>>>>> :
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

Category:

0 comments