YANGA YA KIMATAIFA NI HATAREE ... YAING'OA APR

Unknown | 6:27 PM | 0 comments


YANGA SC imefanikiwa kwenda hatua ya 16 Bora michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika kufuatia kuitoa APR ya Rwanda kwa jumla ya mabao 3-2.
Yanga SC leo imelazimishwa sare ya 1-1 na timu ya jeshi la Rwanda Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam – na kwa kuwa ilishinda 2-1 katika mchezo wa kwanza mjini Kigali wiki iliyopita, inasonga mbele kwa ushindi wa jumla wa 3-2.
Yanga sasa watamenyana na mshindi wa jumla kati ya Al Ahly ya Misri na Recreativo de Libolo ya Angola katika hatua ya 16 Bora. 
Katika mchezo wa leo, APR ndiyo waliokuwa wa kwanza kupata bao dakika ya tatu kupitia kwa Fiston Nkinzingabo aliyefumua shuti kali akimalizia pasi ya Jean Claude Iranzi.

Yanga walifanikiwa kusawazisha bao hilo dakika ya 28 kupitia kwa mshambuliaji wake, Donald Dombo Ngoma aliyefumua shuti la kitaalamu baada ya pasi nzuri ya kiungo Mzimbabwe mwenzake, Thabani Scara Kamusoko.
Kwa ujumla mchezo wa leo, Yanga walicheza kwa kujihami zaidi wakionekana dhahiri kutaka kuulinda ushindi wao wa ugenini.
Na APR ingeongeza juhudi kidogo tu, ingeweza kuwatia simanzi mashabiki wa nyumbani – lakini labda bahati haikuwa yao.
Kikosi cha Yanga leo kilikuwa; Ally Mustafa ‘Barthez’, Mbuyu Twite, Mwinyi Hajji, Kevin Yondan, Vincent Bossou, Pato Ngonyani, Deus Kaseke/Geoffrey Mwashiuya dk70, Thabani Kamusoko, Donald Ngoma, Amissi Tambwe na Haruna Niyonzima/Simon Msuva dk65. 
APR: Jean Claude Ndoli, Rusheshangonga Michael, Rutanga Eric, Rwatubyaye Abdul, Emery Bayisenge, Yannick Mukunzi, Fiston Nkinzingabo/Djihad Bizimana DK46, Benedata Janvier/Bertrand Iradukunda dk88, Issa Bigirimana, Iranzi Jean Claude na Patrick Sibomana. BIN ZUBERY

Share story hii kupitia>>>>>> :
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

Category:

0 comments