IVO MAPUNDA ‘OUT’ MECHI YA WATANI WA JADI!

Unknown | 9:00 AM | 0 comments

      


IVO-MAPUNDANa Baraka Mpenja, Dar es salaam
HABARI mbaya kwa mashabiki wa Simba sc ni kwamba kipa namba moja wa klabu hiyo, Ivo Philip Mapunda amepata majeruhi itakayomuweka nje ya uwanja kwa wiki nne.
Kocha msaidizi wa klabu hiyo, Seleman Abdallah Matola ‘Veron’ amesema kuwa Ivo ameumia kidole chake leo katika mazoezi ya klabu hiyo visiwani Zanzibar  na daktari wa timu amethibitisha.
Mapunda ataikosa mechi ya watani wa jadi oktoba 12 mwaka huu uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.
Hata hivyo, Matola amesema kukosekana kwa Ivo sio tatizo kubwa kwasababu wana makipa wengine kama Hussein Sharif ‘Casillas’ na kipa Peter Manyika ambao wanaweza kufanya kazi vizuri.
Casillas na Manyika walisajiliwa majira ya kiangazi mwaka huu baada ya mnyama kuachana na kipa Mghana Yaw Berko mwishoni mwa msimu uliopita na kubaki na Ivo.
Majeruhi wanazidi kuongezeka Simba ambapo mpaka sasa Jonas Mkude hayuko fiti kucheza kwa sasa ingawa ameshaanza mazoezi mepesi.
Mkenya Pual Kiongera naye aliumia mechi ya jumapili iliyopita dhidi ya Coastal Union na taarifa zilizotoka jana ni kwamba ana majeruhi sugu ya goti.
Ilifahamika kuwa Kiongera naye atakaa nje ya uwanja kwa wiki sita au miezi  miwili.
Naye beki wa kushoto Issa Rashid ‘Baba Ubaya’ anasumbuliwa na majeruhi na hana uhakika wa kucheza mechi ijayo.
Simba imejificha Zanzibar kujiandaa na mechi ijayo ya ligi kuu dhidi ya Polisi Morogoro itayopigwa jumamosi (septemba 27 mwaka huu) uwanja wa Taifa, Dar es salaam.

Share story hii kupitia>>>>>> :
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

Category:

0 comments