AZAM FC YAIBAMIZA RUVU SHOOTING 3 - 0

Unknown | 10:19 PM | 0 comments


AzamFC
Na Baraka Mpenja wa Fullshangwe, Dar es salaam
Tel; 0712461976 au 0764302956
Mechi ya kujaribu matumizi ya tiketi za elektroniki kati ya Azam na Ruvu Shooting iliyofanyika uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es salaam jioni ya leo imemalizika kwa wana Lambalamba kuibuka na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya vijana wa Charles Boniface Mkwasa.
Azam fc ikiwa chini ya kocha mpya,  Mcameroon, Joseph Marius Omog iliandika bao lake la kwanza katika dakika ya 10 kupitia kwa Mshambuliaji wake hatari na nahodha, John Raphael Bocco kufuatia kazi nzuri ya Mganda, Brian Umony .
Dakika ya 30, mshambuliaji wa Azam fc, Raia wa Ivory Coast,  Kipre Herman Tchetche aliandika bao la pili kwa njia ya mkwaju wa penati baada  ya Ayoub Kitala kuurudisha kwa mkono mpira uliokuwa unaelekea nyavuni. .
Hadi dakika 45 za kipindi cha kwanza zinamalizika, Azam fc walikuwa mbele kwa mabao 2-0.
Kipindi hicho cha kwanza, timu zote zilicheza soka la kufundishika,  hivyo kuleta burudani kubwa kwa mashabiki waliojitokeza kutazama mechi hiyo.
Kipindi cha pili timu zote zilifanya mabadiliko kwa takribani vikosi vizima na mshambuliaji mpya wa Azam kutoka Pwani ya Magharibi mwa Afrika, Ivory Coast, Muamad Ismael Kone  alikuwa kivutio baada ya kugusa nyasi za Chamazi.
Kone alionekana kucheza soka zuri na katika dakika ya 57 alifunga bao la tatu na kukamilisha ushindi wa 3-0 leo hii kwa matajiri wa `Ice Cream`..
Refa Israel Mujuni Nkongo alimpa kadi nyekundu beki wa Ruvu na kuifanya timu ya Charles Boniface Mkwasa ‘Master’ imalizie dakika 50 za pambano hilo ikiwa pungufu.
Mechi nyingine ya majaribio itakuwa kati ya Ashanti United na JKT Ruvu ambayo itachezwa Januari Mosi mwakani kwenye uwanja huo huo.
Baada ya Mchezo huo,  kocha Omog alisema ana kazi kubwa ya kufanya kwani timu inapoteza mipira kirahisi, haina kasi na inapopoteza mipira wachezaji wanategeana kukaba.
Alisifia kikosi cha Azam FC kuwa kina wachezaji wenye vipaji vya hali ya juu na akasema hadi utakapofika muda wa kucheza michezo ya kimtaifa anadhani timu itakuwa tayari.
Mchezo wa leo ulikuwa muhimu kwa kocha wa Azam fc kwani alikuwa anakiangalia kikosi chake kinachojiandaa kushiriki mashindano ya kombe la Mapinduzi inayotarajia kuanza januari mosi mwakani.
Mbali na Azam fc, klabu ya Yanga, Simba na Mbeya City zilithibitisha kushiriki michuano hiyo muhimu kwa timu hizo kuandaa vikosi vyao kuelekea ngwe ya pili ya ligi kuu soka Tanzania bara inayotarajia kuanza kushika kasi januari 25 mwakani.
Yanga wao wana kazi kubwa kwani februari mwakani wanaingia katika kibarua cha ligi ya mabingwa barani Afrika.
Wao Ruvu Shooting chini ya kocha mkuu, Charles Boniface Mkwasa `Masta` wanarejea zao kambini kujiandaa na mzunguko wa pili wa ligi kuu Tanzania bara.

Share story hii kupitia>>>>>> :
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

Category:

0 comments