YANGA YAUKARIBIA UBINGWA ... YAIPIGISHA KWATA MGAMBO

Unknown | 7:50 PM | 0 comments

a Prince Akbar, DAR ES SALAAM BIN ZUBERY
YANGA SC imetanua kwapa kileleni mwa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kufuatia ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Mgambo JKT jioni ya leo Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Ushindi huo unaifanya Yanga ifikishe pointi 62 baada ya kucheza mechi 25, ikifuatiwa na Azam FC sasa yenye pointi 58 za mechi 25 pia, wakati Simba SC inaendelea kushika nafasi ya tatu kwa pointi zake 57 za mechi 25.
Katika mchezo huo uliochezeshwa na refa makini wa Mwanza, hadi mapumziko, timu hizo zilikuwa zimefungana bao 1-1, Mgambo wakitangulia na wenyeji Yanga kusawazisha.

Mfungaji wa mabao ya Yanga leo, Deus Kaseke (kushoto) akipongezwa na mchezaji wenzake, Simon Msuva 

Bolly Shaibu aliifungia Mgambo JKT dakika ya nne, akimalizia pasi ya Nassor Gumbo ambaye alimpokonya mpira kiungo wa Yanga, Salum Telela nje kidogo ya boksi baada ya kuanzishiwa na kipa wake, Deo Munishi ‘Dida’.
Yanga walionekana kupoteana baada ya bao hilo la mapema na Gumbo akakaribia kufunga bao la pili dakika ya sita kama si juhudi za kipa Dida.
Hata hivyo, katikati ya kipindi hicho, mabingwa hao watetezi wakatulia na mchezo ukaanza kuwa wa pande zote mbili. 
Yanga ilipata pigo dakika ya 20, baada ya beki wake tegemeo wa kulia, Juma Abdul kuumia na kushindwa kuendelea na mchezo nafasi yake ikichukuliwa na mkongwe, Mbuyu Twite kutoka DRC. 
Kiungo Deus Kaseke akaifungia Yanga bao la kusawazisha dakika ya 43 akimalizia pasi ya kichwa ya Mrundi Amissi Tambwe baada ya krosi nzuri ya juu ya beki wa kushoto, Oscar Joshua.
Winga wa Yanga, Simon Msuva (kushoto) akimtoka beki wa Mgambo JKT leo Uwanja wa Taifa
Mshambuliaji wa Yanga, Amissi Tambwe (kushoto) akikimbilia mpira dhidi ya beki wa Mgambo JKT leo

Almanusra Paul Nonga aifungie Yanga dakika ya 45 baada ya krosi nzuri ya Telela, lakini kichwa cha kudundisha alichopiga kikapaa juu kidogo ya lango.
Yanga wakafanya mashambulizi mengine mawili makali langoni mwa Mgambo dakika mbili za nyongeza, lakini wakaishia kukosa mabao ya wazi.
Kipindi cha pili, koha wa Yanga, Mhoalanz, Hans van der Pluijm alianza kwa mabadiliko, akimpumzisha Nonga na kumuingiza Mzimbabwe Donald Ngoma.
Mabadiliko hayo yaliongeza ubora wa Yanga uwanjani dhidi ya wapinzani na dakika ya 53 Ngoma alipiga nje akiwa anatazama nyavu baada ya krosi ya Msuva.
Bolly Shaibu alikaribia kufunga dakika ya 60 baada ya kuwazidi maarifa mabeki wa Yanga, lakini kipa Dida alitoka na kupambana naye hadi kumharibia mipango yake.
Yanga wakajibu kwa mashambulizi mawili mfululizo, dakika ya 68 kipa Said Hamisi alipangua shuti la papo kwa papo la Deus Kaseke na dakika ya 69 Tambwe akaunganishia nje kwa kichwa krosi ya Telela.
Deus Kaseke tena akawainua vitini wana Yanga dakika ya 72 akimalizia mpira uliookolewa na Bakari Mtama baada ya kichwa cha Tambwe kufutaia krosi nzuri ya Niyonzima.
Kikosi cha Yanga SC kilikuwa; Deo Munishi ‘Dida’, Juma Abdul/Mbuyu Twite dk20, Oscar Joshua, Kevin Yondan, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Salum Telela, Simon Msuva, Haruna Niyonzima/Thabani Kamusoko dk72, Paul Nonga/Donald Ngoma dk46, Amissi Tambwe na Deus Kaseke.
Mgambo JKT; Said Hamisi, Salum Mlima, Chande Magoja, Henry Chacha, Bakari Mtama, Salum Kipaga, Nassor Gumbo/Ally Nassor ‘Ufudu’ dk79, Mohammed Samatta, Herbert Lukindo, Bolly Shaibu na Salum Aziz Gilla.

Share story hii kupitia>>>>>> :
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

Category:

0 comments